Friday, July 23, 2010

Mwisho Arudi kwa Kishindo Big Brother


Nyota ya Mwisho ilianza kung'ara wakati washiriki wa kinyang'anyiro hicho walipowasili katika jumba la Big Brother na kuwafanya watu wengi waliokuwa ndani na nje ya jumba hili kumshangilia kwa nguvu.

Akiwa amevalia nadhifu, koti lililomkaa vyema, akiwa ametupia lubega la kimasai shingoni huku akiwa amevaa hereni katika masikio yake yote mawili, Mwisho alionekana kuwa mwenye furaha na alipoulizwa anajisikiaje namna alivyopokelewa, Mwisho alisema kuwa anashindwa kuelezea.

Mwisho pia alisema kuwa kwa hivi sasa maisha yake anayaendesha kijiji kwao Morogoro, na anafurahia maisha ya huko kwa sababu mbali ya kulima, lakini pia anapata fursa ya kufurahia maisha na wanakijiji.

Watanzania waliohudhuria katika hafla maalumu ya uzinduzi wa shindano hilo, uliofanyika katika hoteli ya Holiday In jijini Dar es Salaam, walifurahishwa na uwakilishi wa Mwisho na kusema kuwa wana matumaini makubwa kuwa atafanya vyema.

"Mwisho ni mshiriki mwenye mvuto kuliko washiriki wote wa Tanzania na tunamatumaini atafanya vyema kama alivyofanya awali," alisema msanii mahiri wa filamu nchini, Jacob Steven 'JB'.

"Siyo siri jamaa anapendwa. Anakubalika kwa kweli. Nyota yake bado iko juu. Mimi nakuambia Mwisho atawafanya watanzania wayafuatilie tena mashindano hayo kwa ukaribu mno." alisema Miss Tanzania Miriam Gerald ambaye alikuwa miongoni mwa wageni waalikwa.

Washiriki walioingia katika jumba hilo ni Paloma Manda kutoka Zambia, Jeniffer Mussanhane (Msumbiji), Dj Code Sangala (Malawi), Samwel Kwame Bampoe 'Sammy B' (Ghana), Maureen Namatovu (Uganda), Jacob Yehdego (Ethiopia), Munyaradzi Hidzonga (Zimbabwe).

Wengine ni Sheila Kwamboka (Kenya), Meryl Shikwambane (Namibia), Uti Nakumbe (Zimbabwe), Lerato Sengadi (Afrika Kusini), Kaone Ranantshonyana (Botswana) na Hannington Kuteesa(US).

No comments:

Post a Comment